Mheshimiwa Samuel Sitta, Mwenyekiti wa Bunge Maalum la Katiba;
Mheshimiwa Dkt. Mohamed Gharib Bilal, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Dkt. Ali Mohamed Shein, Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi;
Mheshimiwa Mizengo Peter Pinda, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Maalim Seif Sharif Hamad, Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar;
Mheshimiwa Balozi Seif Ali Iddi, Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
Mheshimiwa Anne Semamba Makinda; Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano;
Mheshimiwa Pandu Ameir Kificho, Spika wa Baraza la Wawakilishi na Mwenyekiti wa Muda wa Bunge Maalum la Katiba ;
Mheshimiwa Rashid Othman Chande, Jaji Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania;
Mheshimiwa Othman Makungu, Jaji Mkuu wa Zanzibar;
Viongozi Wakuu Wastaafu;
Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge Maalum la Katiba;
Waheshimiwa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba;
Wageni waalikwa;
Mabibi na Mabwana;
Pongezi
Nakushukuru
sana Mheshimiwa Mwenyekiti kwa kunipa fursa ya kuja kuzungumza na
Waheshimiwa Wajumbe wa Bunge letu Maalum la Katiba katika siku hii
muhimu na ya kihistoria kwa nchi yetu. Nimekuja kuwatakia heri na
naungana na Watanzania wenzetu wote kuwaombea baraka za Mwenyezi Mungu,
ili muweze kuifanya kazi yenu kwa utulivu, hekima, umakini mkubwa na
kuimaliza kwa salama na kwa mafanikio yanayoyatarajiwa na Watanzania.
Natoa
pongezi nyingi kwako na kwa Makamu wako kwa kuchaguliwa kwenu kuongoza
Bunge hili maalumu na la kihistoria. Ushindi mkubwa mliopata ni
kielelezo tosha cha imani kubwa na matumaini waliyonayo Wajumbe wenzenu
kwenu. Matumaini yao ndiyo matumaini ya Watanzania wote, kwamba
mtaliongoza vizuri Bunge hili, ili liweze kutimiza kwa ufanisi mkubwa
jukumu lake muhimu sana katika historia ya Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Niruhusu
pia niwapongeze kwa dhati Wajumbe wote wa Bunge Maalum la Katiba kwa
bahati ya aina yake waliyopata ya kutunga Katiba mpya ya Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania. Fursa hii hutokea mara chache sana katika historia
ya nchi yo yote na watu wake. Mkifanikiwa kuipatia nchi yetu Katiba
nzuri majina yenu yataandikwa kwa wino wa dhahabu, katika kumbukumbu za
historia ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Ni
matarajio ya Watanzania kuwa mtatunga Katiba itakayokubalika na wengi.
Katiba inayotekelezeka. Katiba itakayoimarisha Muungano wetu kwa kuondoa
changamoto zilizopo sasa. Katiba itakayoipa nchi yetu mfumo bora wa
kuongoza na kuendesha mambo yetu. Katiba itakayoimarisha umoja, upendo,
ushirikiano na mshikamano miongoni mwa wananchi wa Tanzania, licha ya
tofauti zao za asili za upande wa Muungano na maeneo watokako, au
tofauti za jinsia, rangi, kabila, dini na ufuasi wa vyama vya siasa.
Katiba itakayodumisha amani, usalama na utulivu nchini. Katiba
itakayostawisha zaidi demokrasia, haki za binadamu, utawala wa sheria,
utawala bora na kudhibiti maovu.
Na,
mwisho ingawaje siyo mwisho kwa umuhimu, Katiba itakayoweka mazingira
mazuri kwa uchumi wa nchi kukua, na wananchi wengi kunufaika sawia na
maendeleo yatayopatikana.
Historia ya Katiba Nchini
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe;
Hii
itakuwa mara ya tatu tangu kuzaliwa kwa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
Aprili 26, 1964, kwa nchi yetu kuwa na mchakato wa kutunga Katiba mpya.
Mara ya kwanza ilikuwa mwaka 1965 ilipotungwa Katiba ya Muda na mara ya
pili ni mwaka 1977 ilipotungwa Katiba ya Kudumu tuliyonao sasa. Tofauti
na mara mbili zilizopita, safari hii mchakato unahusisha watu wengi
zaidi. Wananchi wameshiriki moja kwa moja kutoa maoni yao kwa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba, na ndio watakaofanya uamuzi wa mwisho kuhusu
Katiba mpya kwa kura ya maoni. Wananchi pia walipata nafasi ya kuchagua
Wajumbe wa Mabaraza ya Katiba ya Wilaya yaliyojadili Rasimu ya Kwanza ya
Katiba. Pia walipata nafasi ya kutoa maoni yao kupitia Mabaraza ya
Katiba ya taasisi. Katika Bunge hili wapo wananchi 201 kutoka makundi
mbalimbali.
Katika
mchakato wa kutunga Katiba za mwaka 1965 na 1977 kulikuwapo Tume za
Kuandaa Rasimu na Bunge Maalum la Katiba kama ilivyo katika mchakato
huu. Hata hivyo, kwa Katiba zilizopita Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya
Muungano pekee ndio waliounda Bunge Maalum. Safari hii Bunge Maalum
linajumuisha Wabunge, Wajumbe wa Baraza la Wawakilishi na wananchi 201
wanaotoka kwenye jamii, wakiwakilisha asasi na makundi mbalimbali ya
Watanzania kutoka Zanzibar na Tanzania Bara. Mchakato wa sasa utaishia
kwenye kura ya maoni itakayoshirikisha wananchi wote wa Tanzania
wanaoruhusiwa kupiga kura. Michakato iliyopita iliishia Bunge Maalum
pekee.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tangu
kutungwa kwake, tarehe 25 Aprili, 1977, mpaka sasa Katiba ya Jamhuri ya
Muungano ya mwaka 1977 imefanyiwa mabadiliko takriban mara 14.
Mabadiliko hayo yalitokana na kufanyika au kutokea kwa mabadiliko muhimu
ya kiuchumi, kisiasa na kijamii katika nyakati mbalimbali hapa nchini
na katika Jumuiya ya Afrika Mashariki.
Kwa ruksa yako naomba nitaje baadhi ya mabadiliko yaliyofanywa:-
Mabadiliko
ya 1979 yaliunda Mahakama ya Rufani ya Tanzania kufuatia kufa kwa
Mahakama ya Rufani ya Afrika Mashariki baada ya kuvunjika kwa Jumuiya ya
Afrika Mashariki mwaka 1977.
Mabadiliko
ya mwaka 1980 yalifanyika baada ya kutungwa kwa Katiba ya Zanzibar,
hivyo kulazimu Katiba hiyo kutambulika kwenye Katiba ya Jamhuri ya
Muungano
Mabadiliko
ya mwaka 1984 yaliweka utaratibu wa ukomo wa vipindi vya Urais ambao
haukuwepo kabla ya hapo. Aidha, masuala ya Haki za Binadamu (Bill of
Rights) yaliingizwa kwa mara ya kwanza katika Katiba. Vilevile, Mahakama
ya Rufani ya Tanzania na mambo mengine ya iliyokuwa Jumuiya ya Afrika
Mashariki yaliongezwa katika Orodha ya Mambo ya Muungano.
Mwaka
1992, yalifanyika mabadiliko yaliyoanzisha Mfumo wa Vyama Vingi vya
Siasa badala ya ule wa Chama kimoja uliokuwepo tangu 1965. Pia utaratibu
wa uchaguzi wa Rais na Wabunge ulirekebishwa ili uendane na mfumo wa
vyama vingi vya siasa. Vilevile utaratibu wa kuwa na viti maalum vya
wanawake katika Bunge ulianzishwa. Wakati ule ilikuwa asilimia 15 ya
Wabunge wote. Aidha, kwa mara ya kwanza katika historia ya nchi yetu
Bunge lilipewa mamlaka ya kumwajibisha Rais na Waziri Mkuu kupitia kura
ya kutokuwa na imani.
Mabadiliko ya mwaka 1994 yaliweka mfumo mpya wa kumpata Makamu wa Rais kupitia Mgombea Mwenza.
Mwaka
2000 na 2005, pamoja na mambo mengine yalifanyika mabadiliko yaliyopanua
wigo wa Haki za Binadamu na kuongeza uwakilishi wa wanawake.
Umuhimu wa Mabadiliko ya Katiba
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kufanyika
kwa mabadiliko hayo kunathibitisha utayari wa Serikali kufanya
mabadiliko kila ilipoonekana inafaa kufanya hivyo. Pamoja na kufanya
yote hayo na Serikali kuwa na msimamo huo, kumekuwepo na madai
yaliyokuwa yanajirudia ya kutaka Katiba ya Tanzania iandikwe upya. Wako
watu walioimithilisha Katiba yetu na nguo yenye viraka vingi mno kiasi
kwamba ingefaa kununua mpya badala ya kuendelea kuivaa.
Madai ya
kutaka Katiba mpya yalipazwa sauti baada ya kuanza kwa mfumo wa vyama
vingi vya siasa. Wapo waliokuwa wanadai Katiba mpya kwa imani, eti
kwamba, itawawezesha kuishinda CCM. Lakini, si hayo tu, hata katika
mchakato wa Serikali zetu mbili kushughulikia kero za Muungano,
imedhihirika kuwa baadhi ya changamoto zilikuwa zinahitaji mabadiliko ya
Katiba ili kuzipatia ufumbuzi wa uhakika na wa kudumu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa
kutambua ukweli huo na baada ya kushauriana na kukubaliana na viongozi
wenzangu wakuu wa Chama tawala na Serikali zetu mbili wakati ule, ndipo
tarehe 31 Desemba, 2010, nikatangaza dhamira ya kuanzisha mchakato wa
kutunga Katiba mpya. Nilieleza siku ile kuwa katika mchakato huo
tutakuwa na ushirikishwaji mpana wa wananchi wa Tanzania kwa makundi yao
ya jinsia, dini, siasa na shughuli wazifanyazo kujipatia riziki na kwa
maeneo wanayotoka katika pande zetu mbili za Muungano.
Mchakato wa Katiba Mpya
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tarehe 16
Machi, 2011 Baraza la Mawaziri liliridhia kutungwa kwa Sheria ya
Mabadiliko ya Katiba ya kuliongoza taifa katika mchakato wa kutunga
Katiba mpya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Tarehe 18 Novemba, 2011
Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilipitisha Muswada wa Sheria
ya Mabadiliko ya Katiba. Kwa mujibu wa Sheria hiyo, mchakato wa kutunga
Katiba Mpya ulikuwa unaanza kwa kuunda Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Tume hiyo imepewa jukumu la kusikiliza maoni ya wananchi mmoja mmoja na
kwa makundi yao ya maslahi, taasisi zao na kupitia Mabaraza ya Katiba.
Mwishowe Tume imetakiwa kutengeneza Rasimu ya Katiba mpya
itakayofikishwa kwenye Bunge Maalum la Katiba kujadiliwa na Katiba mpya
kutungwa. Mchakato wa Katiba utahitimishwa kwa wananchi kupiga kura ya
maoni ya kuamua kama wanaikubali au kuikataa Katiba mpya.
Tarehe 6
Aprili, 2012 nilifanya uteuzi wa Wajumbe wa Tume ya Mabadiliko ya Katiba
na kuwaapisha tarehe 13 Aprili, 2012. Tume ilianza kazi tarehe 2 Mei,
2012 na kuikamilisha kwa mafanikio, hatua zote zilizoihusu na kukabidhi
kwangu na kwa Rais wa Zanzibar, Taarifa ya Tume na Rasimu ya Katiba
tarehe 30 Desemba, 2013. Kitendo cha Mwenyekiti wa Tume, Mheshimiwa
Joseph Warioba kuwasilisha Rasimu hiyo mbele ya Bunge hili tukufu tarehe
18 Machi, 2014, kinahitimisha rasmi kazi ya Tume ya Mabadiliko ya
Katiba. Kazi inayofuatia ni ya Bunge hili kujadili, kuamua na kutunga
Katiba mpya. Baada ya hapo Katiba mpya itafikishwa kwa wananchi kwa
uamuzi wa mwisho kwa njia ya kupiga kura ya NDIYO au HAPANA.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Rasimu ya
Katiba ilichapishwa kwenye gazeti la Serikali na magazeti mengine
yanayosomwa na wananchi kama ilivyoagizwa katika Kifungu cha 20(2) cha
Sheria ya Mabadiliko ya Katiba. Pamoja na hayo, Taarifa ya Tume na
Rasimu ya Katiba viliwekwa wazi kwenye tovuti ya Tume kwa kila mtu
kusoma. Inafurahisha kuona kuwa watu wengi wameisoma Taarifa ya Tume na
Rasimu ya Katiba na kumekuwa na mjadala mpana kuhusu nyaraka zote hizo
muhimu. Watu wengi wametoa maoni yao na wanaendelea kufanya hivyo. Kwa
maoni yangu hili ni jambo jema sana na ni kielelezo thabiti kuwa
demokrasia imestawi na inazidi kuota mizizi Tanzania. Pia, kwamba,
Watanzania wako huru kushiriki na kutoa maoni yao kwa mambo
yanayowahusu.
Pongezi kwa Tume
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa mara
nyingine tena narudia kutoa pongezi za dhati kwa Wajumbe wa Tume ya
Mabadiliko ya Katiba chini ya uongozi wa Mheshimiwa Jaji Joseph Warioba
akisaidiwa na Mheshimiwa Jaji Augustino Ramadhani, kwa kazi kubwa na
nzuri waliyofanya. Kazi yao haikuwa rahisi hasa ukizingatia ukubwa wa
nchi yetu, wingi wa watu wake, utitiri wa taasisi na pigo la kumpoteza
Mjumbe mwenzao muhimu Dkt. Sengondo Mvungi aliyetangulia mbele ya haki
katikati ya mchakato.
Pamoja na
hayo, kwa bidii kubwa Wajumbe wa Tume wameweza kutembelea mikoa yote
nchini na kuwafikia watu 351,644 waliotoa maoni yao kwa mdomo na kwa
maandishi. Halikadhalika, walipokea na kuchambua maoni 772,211 kutoka
kwa wananchi na taasisi mbalimbali. Baada ya kupokea maoni ya wananchi,
kufanya utafiti na kwa kutumia maarifa na uzoefu wao, Wajumbe wakafanya
kazi ngumu, kuliko yote, ya kutengeneza Rasimu ya Katiba iliyoko mbele
ya Bunge hili. Ni kweli kwamba Wajumbe hawakuweza kuwafikia wananchi
wote wa Tanzania, lakini wameweza kuwafikia wananchi wengi, ambao kwa
kiasi kikubwa wanawakilisha taswira na mitazamo mipana ya jamii yetu.
Baadhi ya Masuala Yaliyojitokeza Katika Mjadala wa Mapendekezo ya Tume
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tume
imefanya kazi nzuri, yenye thamani kubwa na ya manufaa kwa taifa la
Tanzania. Rasimu imeandikwa vizuri na kwa weledi wa hali juu. Tume
imetoa mapendekezo ambayo kwa kiasi kikubwa yanahuisha na kuboresha
Katiba ya nchi yetu, kwa namna ya pekee. Katiba inayopendekezwa,
imejumuisha dhana na mambo kadhaa mapya yanayokwenda vyema na wakati
tulionao na kuweka msingi mzuri kwa huko mbele tuendako. Kwa taratibu za
kawaida za marekebisho ya Katiba tuliyonayo, isingekuwa rahisi kuingiza
mambo mengi mapya kiasi hiki.
Wajumbe Wana Kazi Kubwa
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Waheshimiwa Wajumbe;
Rasimu ya
Katiba ni kitabu kikubwa kilichosheheni mambo mengi. Kina kurasa 106,
sura 17 na ibara 271. Wajumbe wa Bunge hili mnatakiwa kusoma na kuelewa
vizuri kila kilichoandikwa ili muweze kufanya uamuzi ulio sahihi.
Mnawajibika kuchambua kwa kina na umakini mkubwa kila kilichomo, sura
kwa sura, ibara kwa ibara, sentensi kwa sentensi na hata neno kwa neno.
Hamna budi kujiridhisha kuhusu uandishi wa vifungu vya Rasimu ya Katiba
na kufaa kwa dhana mbalimbali zilizoingizwa na kujengeka katika Rasimu.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kile
ambacho Wajumbe mtaona kinastahili kuboreshwa au kurekebishwa au kufutwa
msisite kufanya hivyo ili Watanzania wapate Katiba iliyo bora.
Msipofanya hivyo kuna hatari ya kupata Katiba ambayo ni ngumu
kuitekeleza. Aidha, tunaweza kuwa na Katiba ambayo itanung'unikiwa na
watu wengi na kusababisha madai ya kutaka ifanyiwe marekebisho muda
mfupi baada ya kupitishwa. Bunge hili linao wajibu maalum wa kuzuia
balaa hilo lisitokee katika nchi yetu. Ngazi mbalimbali zilizowekwa
katika mchakato huu ni kama chujio la kuepusha hali hiyo isitokee. Kile
ambacho hakikuonekana katika hatua moja kitaonekana katika hatua
inayofuata na kurekebishwa. Nawaomba fursa mliyonayo muitumie vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Nimekwishaeleza
kuwa moja ya jambo mnalotegemewa kufanya ninyi wenzetu mliopewa dhamana
ya kutunga Katiba ya nchi yetu ni kujiridhisha na uandishi wake. Yapo
maoni yaliyotolewa kuhusu uandishi ambayo naomba myatafakari na kuamua
ipasavyo. Kwa mfano, kuna baadhi ya vifungu vya Katiba vinayopendekezwa
vimekuwa na mambo mengi mno kuliko inavyostahili Katiba kuwa (too
prescriptive). Pia kuna mawazo kwamba baadhi ya mambo hayangetakiwa kuwa
katika Katiba bali yawe kwenye Sheria zinazotafsiri utekelezaji wa
Katiba yenyewe.
Yako
mambo yaliyotajwa kwenye Katiba ambayo yanatakiwa kuelezwa wazi kuwa mtu
hatakwenda mahakamani kuidai Serikali impatie (non justiciable). Mambo
yaliyotajwa kwenye Katiba ni mazuri na yanavutia, lakini lazima yaendane
na uwezo wa nchi na uchumi wake kuhimili. Simaanishi kwamba tuyatoe
kwenye Katiba, bali yabakie kama dhamira pale uwezo wa nchi
utakaporuhusu yatekelezwe. Tusipofanya hivyo, kuna hatari ya Serikali
kujikuta inalaumiwa au hata kufikishwa mahakamani kila wakati kwa madai
ya jambo moja au jingine ambayo haina uwezo nayo. Ni muhimu sana mambo
kama hayo muyatazame ili tusije kuwa na Katiba ambayo ni ngumu
kutekeleza.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Yapo pia
maoni kuwa baadhi ya vifungu vina upungufu katika uandishi wake, hivyo
kuhitaji kufanyiwa marekebisho. Isipofanyika hivyo kunaweza kuwepo
athari na nyingine zinaweza kuwa mbaya. Kwa mfano, Ibara ya 2 ya Rasimu
inayotambulisha eneo na mipaka ya nchi yetu. Ibara hiyo inasomeka kuwa
"Eneo la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni eneo lote la Tanganyika
likijumuisha sehemu yake ya bahari na eneo lote la Zanzibar likijumuisha
sehemu yake ya bahari".
Maelezo
hayo yameacha kutambua, kwa upande wa Tanzania Bara, sehemu yetu ya
maziwa na mito ambayo ni kubwa sana. Kwa nini tuache kuitaja? Je hatutoi
nafasi kwa nchi tunazopakana nazo siku moja wakaja kupora sehemu zetu
hizo na sisi kukosa utetezi kwa kuwa hata Katiba yetu haikuyatambua
maeneo hayo kuwa ni yetu? Hili ni jambo kubwa ambalo Bunge hili lazima
mlirekebishe. Wakati ndiyo huu hakuna mwingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo
jingine kuhusu uandishi ni mgongano kati ya pendekezo la msingi la Tume
la kuwa na muundo wa Serikali tatu na majukumu ya Serikali ya Muungano
ambayo kimsingi ni majukumu ya Serikali za nchi washirika. Katika Rasimu
hii malengo ya taifa yameainishwa na Serikali ya Muungano inatakiwa
kuhakikisha kuwa malengo hayo yanatekelezwa na itoe taarifa Bungeni.
Katika mfumo wa Serikali tatu unaopendekezwa na Tume masuala yahusuyo
uchumi na maendeleo ya jamii kama vile kukuza kilimo, ufugaji, uvuvi,
viwanda, biashara, pembejeo, elimu, hifadhi ya jamii na kadhalika yako
chini ya mamlaka ya Serikali za nchi washirika. Mamlaka ya Serikali ya
Muungano ni kwa mambo saba tu yafuatayo:- Katiba na Mamlaka ya Jamhuri
ya Muungano, Ulinzi na Usalama wa Jamhuri ya Muungano, Uraia na
Uhamiaji, Sarafu na Benki Kuu, Mambo ya Nje, Usajili wa Vyama vya Siasa,
Ushuru wa Bidhaa na Mapato yasiyo ya kodi yatokanayo na Mambo ya
Muungano.
Kwa
Rasimu kupendekeza muundo wa Serikali tatu na kuipa Serikali ya Muungano
majukumu ambayo haina mamlaka nayo, ni kuzusha utata na migongano kati
ya Serikali ya Muungano na nchi washirika. Mkichagua mfumo wa Serikali
tatu, inawalazimu muyaondoe mambo hayo kwani Serikali ya Muungano
haistahili kuyatekeleza na wala haina uwezo wa kuweka masharti kwa
Serikali za nchi washirika kwa mambo yaliyo kwenye mamlaka ya nchi hizo.
Lakini kama mtaamua tuendelee na muundo wa Serikali mbili, mambo haya
mazuri yanatekelezeka na Serikali ya Muungano bila ya matatizo. Katika
uandishi wa Rasimu Utumishi katika Serikali ya Muungano haumo katika
Orodha ya Mambo ya Muungano. Ni lazima liwemo. Hayo ni baadhi tu ya
masuala yahusuyo uandishi katika Rasimu. Naamini mkiisoma Rasimu kwa
makini mnaweza kuyagundua mengineyo.
Dhana Mpya
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika
Rasimu kuna dhana mpya na mambo mapya kadhaa yaliyoingizwa ambayo
yanabadili utaratibu wa sasa wa uendeshaji wa nchi na mambo mbalimbali.
Nawaomba mfanye uchambuzi wa kina kwa kila kinachopendekezwa na
kujiridhisha kuhusu kufaa kwake na manufaa yake. Fanyeni hivyo ili
tujihakikishie kuwepo kwa mambo mazuri na uendeshaji mzuri wa shughuli
katika taifa letu changa.
Mambo ni
mengi na kwa ufinyu wa muda sitaweza kuyazungumzia yote. Niruhusuni
nizungumzie baadhi ya dhana na mambo mapya yaliyomo katika Rasimu. Jambo
la kwanza, kwa mfano, linahusu Ibara ya 128 (2)(d) inayoleta dhana ya
"Mbunge kupoteza Ubunge iwapo atashindwa kufanya kazi za Mbunge kwa
miezi sita mfululizo kutokana na maradhi au kizuizi ndani ya gereza".
Watu
hawana tatizo na Mbunge kuwa kizuizini ndani ya gereza kama amepatikana
na hatia Mahakamani na kuhukumiwa kifungo. Lakini, isijekuwa yuko
rumande kwa tuhuma akisubiri kesi kusikilizwa. Je akija kuonekana hana
hatia na kuachiliwa? Naungana na wale wanaoshauri kuwa jambo hili
lifafanuliwe vizuri na kutambua Mbunge kutiwa hatiani na kupata adhabu
ya kifungo cha kipindi hicho. Ni bora ifanyike hivyo sasa ili kuondoa
mikanganyiko. Hakuna haja ya kusubiri mpaka jambo hili lije kufafanuliwa
baadaye kwa Sheria itakayotungwa na Bunge.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Kwa
upande wa mtu kupoteza Ubunge kwa sababu ya "kuugua kwa miezi sita
mfululizo" ni maoni ya watu wengi kuwa huu ni ukatili ambao haustahili
kufanywa na Katiba. Kuugua ndiyo ubinadamu na wakati mwingine Mbunge
anaweza kupata ajali akiwatumikia wananchi wa Jimbo lake. Anaweza kuugua
kwa miezi sita au zaidi na kupona kabla ya kipindi chake cha Ubunge
kufika mwisho. Kwa nini awekewe ukomo wa miezi sita? Katiba ya mwaka
1977 tunayotumia sasa haina sharti hilo. Watu wanauliza hoja na haja ya
kuwa na sharti hili kwenye Katiba mpya ni ipi? Wanasema kwa kweli
anachostahili Mbunge huyu kufanyiwa ni kuuguzwa afya yake iimarike ili
aendelee kutumikia watu wake, na siyo kupoteza uongozi wake. Tusiwatie
watu kishawishi cha kukatiza matibabu ili kukwepa sharti hilo. Ni vyema
jambo hili mkalitazama kwa makini, na muone kama linastahili kuwepo au
hapana.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Katika
Rasimu hii imeingizwa dhana mpya ya kuweka ukomo wa vipindi vitatu kwa
Wabunge. Tena mapendekezo haya hayasemi vipindi vitatu mfululizo au la!.
Jambo hilo limezua mjadala motomoto katika jamii. Ni vizuri
mkajiridhisha juu ya sababu za msingi na manufaa ya kufanya hivyo hapa
Tanzania. Mazoea yetu na ya kwingineko duniani ni kuweka ukomo kwa Wakuu
wa Nchi kwa sababu nzuri na rahisi kuzielezea. Lakini, kuwawekea ukomo
Wabunge ni jambo jipya na huenda Tanzania tukawa wa kwanza. Nashawishika
kuungana na wale wanaopendekeza kuwa pengine ni mapema mno kuanzisha
utaratibu huo hapa kwetu.
Nachelea
kuwa tutainyima nchi yetu fursa ya kupata watu wenye maarifa na uzoefu
mzuri wa uongozi kwa nafasi ya Ubunge au kwa nafasi za uongozi wa Taifa
bila ya sababu za msingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo
lingine jipya linalopendekezwa na Tume ni utaratibu wa kumuondoa Mbunge
katikati ya kipindi chake cha uongozi. Kwa hoja linaonekana kuwa jambo
jema lakini naomba athari zake mzitafakari vizuri. Kuna hatari ya
kuanzisha misuguano kwenye Majimbo na kuwaacha Wabunge wasifanye kazi
zao kwa utulivu bali wawe wanajihami dhidi ya wapinzani wao
kuwatengenezea fitna za kuwatoa. Utaratibu unaopendekezwa wa Chama chake
kujaza nafasi ya Mbunge inapokuwa wazi katika mazingira hayo nao
unaweza kuwa ndicho kichocheo kikubwa cha vuguvugu la kumuondoa Mbunge.
Walioshindwa kwenye kura ya maoni wanaweza kufanya kazi ya kuwachimba
wenzao mpaka waondoke. Jipeni muda wa kupima faida na hasa thamani
inayoongezwa na kuanzisha utaratibu huo. Naomba tujiridhishe kama jambo
hili jipya lina tija. Hivi kupewa nafasi kila miaka mitano kurudi kwa
wananchi hakutoshi kumuondoa Mbunge ambaye watu wamemchoka?
Muundo wa Muungano
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Jambo
lingine kubwa lililopendekezwa na Tume ambalo limevuta hisia za karibu
watu wote nchini linahusu muundo wa Muungano wetu kuwa wa Serikali tatu
badala ya mbili za sasa. Pendekezo hili limezua mjadala mkubwa tangu
lilipotolewa katika Rasimu ya kwanza na kurudiwa katika Rasimu ya pili.
Wakati mwingine mjadala umekuwa mkali na wa hisia kali kwa kila upande.
Kwa kweli
hili ndilo jambo kubwa kuliko yote katika Rasimu kwa sababu
linapendekeza kuanzishwa kwa muundo na mfumo mpya wa kuendesha nchi
yetu. Hii ndiyo agenda mama ya Bunge hili ambayo kila Mtanzania
anasubiri kwa hamu uamuzi wenu utakuwa upi. Ombi langu kwenu ni kuwa
watulivu mnapojadili suala hili. Epukeni jazba ili mfanye uamuzi ulio
sahihi. Lazima mtambue uamuzi usiokuwa sahihi kwa jambo hili una hasara
kubwa. Tunaweza kupoteza kitu tulichokijenga kwa gharama kubwa kwa nusu
karne iliyopita. Tanzania inaweza kuwa nchi iliyojaa migogoro na
matatizo mengi ambayo hatunayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wajumbe;
Kama
alivyoeleza Mwenyekiti wa Tume Mheshimiwa Jaji Joseph Sinde Warioba,
mara kadhaa, mjadala au madai ya kutaka muundo wa Serikali tatu si jambo
jipya. Ulikuwepo hata wakati wa mazungumzo ya kuunganisha nchi zetu
mbili mwaka 1964. Ulikuwa kiini cha kuchafuka kwa hali ya hewa ya
kisiasa Zanzibar mwaka 1984. Muundo huu uliwahi kupendekezwa na Tume ya
Nyalali mwaka 1992, ndiyo hoja ya G55 mwaka 1993 na umependekezwa pia na
Tume ya Jaji Kisanga ya mwaka 1998. Lakini mara zote hizo mapendekezo
hayo hayakukubaliwa.
Waasisi
wa taifa letu, yaani Mwalimu Julius Nyerere, aliyekuwa Rais wa Jamhuri
ya Tanganyika wakati ule na Sheikh Abeid Amani Karume, aliyekuwa Rais wa
Jamhuri ya Watu wa Zanzibar wakati ule, waliamua kuchagua Muungano wa
Serikali mbili tulionao sasa. Walitoa sababu mbili kuu: "ni muundo
unaoihakikishia Zanzibar kuwa haimezwi na Tanganyika; na pia unaiepusha
Tanganyika kubeba mzigo mkubwa wa kugharamia Serikali ya Tanganyika na
ile ya Muungano".
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Natambua
kuwepo kwa rai ya kutaka Mwalimu Nyerere asitumiwe katika mjadala huu.
Nionavyo mimi ni vigumu kuacha kujadili fikra za Mwalimu Nyerere na
Sheikh Karume katika jambo hili. Wao ndiyo wa mwanzo kujadili na
kukubaliana kuwa mfumo wa Serikali mbili ndiyo bora kwa nchi yetu. Iweje
leo tunapozungumzia kuubadili, mawazo yao yawe hayafai kutumika au hata
kuzungumzwa. Hivi hasa mawazo ya nani pekee ndiyo bora zaidi kutumika?
Tutakuwa hatuutendei haki mjadala huu na sisi wenyewe tunaoshiriki
katika mchakato huu. Rai yangu kwenu ni kuwa mzitazame hoja zote kwa
marefu na mapana yake ili mpime kama zipo sababu za kuubadili muundo wa
sasa wa Muungano wa Serikali mbili na kuleta wa Serikali tatu. Na, kama
zipo mabadiliko hayo yaweje! Lazima mfanye uamuzi kwa utambuzi na hoja
zenye mashiko. (you must make an informed decision).
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Tume
imetoa sababu mbili kubwa za kupendekeza muundo wa Serikali tatu. Sababu
ya kwanza ni kwamba ndiyo matakwa ya Watanzania wengi kote Zanzibar na
Tanzania Bara. Inaeleza kuwa idadi kubwa ya Watanzania waliotoa maoni,
yaani asilimia 60.2 wa kutoka Zanzibar wanaunga mkono muundo wa Serikali
ya Mkataba, na asilimia 61.3 wa kutoka Tanzania Bara wanaunga mkono
muundo wa Serikali tatu. Sababu ya pili ni kwamba muundo huo unatoa
majawabu ya uhakika na endelevu kwa changamoto za muundo wa sasa wa
Serikali mbili zinazonung'unikiwa na watu wa pande zetu mbili za
Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Sababu
hizi mbili kuu zilizotolewa na Tume zimezua mjadala mkali katika jamii.
Wapo wanaokubaliana na Tume na wapo wasiokubaliana nayo. Wapo wanaosema
Tume imesema kweli kwamba Watanzania wengi wanaunga mkono muundo wa
Serikali tatu, hivyo muundo wa Serikali tatu hauepukiki. Ndiyo matakwa
ya wengi hivyo msemo wa Kiswahili usemao wengi wape uheshimiwe.
Lakini
wapo wanaodai kuwa takwimu za Tume hazionyeshi ukweli huo. Wanasema kuwa
taarifa ya Tume imeonesha kuwa Watanzania waliotoa maoni yao kwa Tume
kwa mdomo na maandishi walikuwa 351,664. Kati yao ni wananchi 47,820 au
sawa na asilimia 13.6 ndiyo waliokerwa na muundo wa Muungano hivyo
wakauzungumzia. Wananchi 303,844 au sawa na asilimia 86.4 muundo wa
Muungano kwao halikuwa tatizo, ndiyo maana hawakuuzungumzia kabisa.
Wanahoji kuwa iweje leo asilimia 13.6 ya Watanzania wote waliotoa maoni
wageuke kuwa ndiyo Watanzania walio wengi!
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Wanasema
pia, kwamba mbona Taarifa ya Tume yenyewe, kuhusu takwimu (uk. 66 na
67), inaonesha kwamba kati ya hao watu 47,820 waliotoa maoni kuhusu
Muungano, ni watu 17,280 tu ambao ni sawa na asilimia 37.2 ndiyo
waliotaka muundo wa Serikali tatu, asilimia 29.8 walitaka Serikali
mbili, asilimia 25.3 walipendekeza Serikali ya Mkataba na asilimia 7.7
walipendekeza Serikali moja. Hii hoja ya Watanzania wengi kutaka
Serikali tatu msingi wake upi?
Mheshimiwa Mwenyekiti;
Takwimu
za Tume (uk. 57) zinaonyesha, vilevile kuwa Tume ilipokea maoni 772,211.
Kati ya hayo asilimia 10.4 tu ndiyo yaliyozungumzia muundo wa Muungano
na asilimia 88.6 hayakuzungumzia Muungano bali mambo mengine. Hivyo basi
wanahoji pia kwamba kama muundo wa Muungano ungekuwa ni jambo
linalowakera Watanzania wengi, lingedhihirika kwenye idadi ya watu
waliotoa maoni na kwenye idadi ya maoni yaliyotolewa. Yote hayo
hayakujitokeza. Waliouzungumzia Muungano walikuwa asilimia 13.6 tu ya
watu wote waliotoa maoni na maoni yanayohusu Muungano yalikuwa asilimia
10.4 ya maoni yote. Hivyo basi, wanauliza "usahihi wa hoja ya Watanzania
wengi kutaka Serikali tatu uko wapi?"
Changamoto za Muundo wa Serikali Mbili
Mheshimiwa Mwenyekiti na Waheshimiwa Wajumbe;
Kama
nilivyokwishagusia awali, sababu ya pili ambayo Tume inatoa kuhusu kufaa
kwa muundo wa Serikali tatu ni kwamba mfumo huu unajibu changamoto
nyingi za muundo wa Serikali mbili. Tume imeainisha vizuri changamoto za
muundo wa Serikali mbili. Kwa upande wa Zanzibar wanalalamikia kile
kinachoitwa Tanzania Bara kuvaa koti la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania
na hivyo kutumia mamlaka ya Serikali ya Muungano kujinufaisha yenyewe.
Fursa hiyo Zanzibar hainayo. Aidha, wanasema mipaka na mamlaka ya
Serikali ya Muungano kwa mambo ya Muungano, na kwa mambo ya Tanzania
Bara haijaainishwa vizuri ikaeleweka. Wazanzibari pia, wanazungumzia
mkanganyiko kuhusu ugawanaji wa mapato, na jinsi ya kuchangia shughuli
za Muungano baina ya Serikali ya Muungano na Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar. Vilevile, wanalalamikia Rais wa Zanzibar kuondolewa kuwa
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano.
Aidha, kuna malalamiko kuwa orodha ya mambo ya Muungan