Ijumaa, 4 Aprili 2014

ZUIO LA BODABODA KATIKATI YA JIJI LA DAR ES LAAM LIANGALIWE UPYA


DSC 0054 7befc
Kumeibuka sintofahamu kubwa katika maeneo ya katikati ya jiji la Dar es Salaam.
Hii ni kati ya wananchi wanaotumia usafiri wa pikipiki kwa ajili ya kuwahi maeneo yao ya kazi na askari wa kikosi cha usalama barabarani wanaosaidiana na maafisa wa kampuni moja binafsi iliyopewa jukumu la kuhakikisha kwamba amri ya kuzuia vyombo hivyo ingali ikitekelezwa.(Hudugu Ng'amilo)
Tayari kumeibuka malalamiko mengi kuhusiana na amri hiyo inayodaiwa kubarikiwa na Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Mkoa, kwa kile kinachoelezwa kuwa ni njia mojawapo ya kupunguza vitendo vya uhalifu kama ujambazi katika maeneo ya katikati ya jiji la Dar es Salaam.
Wapo wananchi wanaolalamikia uwapo wa faini zisizokuwa na ukomo, baadhi zikifikia hadi Sh. 50,000. Wapo wanaolia kwa kudai kukumbana na adha za kuombwa rushwa waziwazi. Kuna malalamiko vilevile yanayohusiana na ubabe uliokithiri
Wengine wanalalamika kuwa, utekelezaji wa zuio la bodaboda umekuwa chanzo cha usumbufu kwani waliopewa jukumu hilo hushindwa kutofautisha wenye bodaboda na raia wa kawaida wanaotumia pikipiki kwa matumizi yao binafsi na familia zao.
Kimsingi, sisi hatukubaliani na utaratibu unaotumika sasa. Tunadhani kwamba, hata kama kulikuwa na dhamira nzuri, lakini kinachoonekana ni kero dhidi ya wananchi.
Kwa mfano, NIPASHE tunaona kuwa uamuzi wa kuzuia bodaboda kwenye maeneo ya katikati ya jiji la Dar es Salaam haujatolewa katika kipindi sahihi.
Hii ni kutokana na ukweli kuwa hivi sasa, wakazi wa Dar es Salaam wako katika kipindi kigumu cha mpito, wakishuhudia miradi mikubwa ya ujenzi wa barabara iliyosababisha maeneo mengi kutopitika kirahisi.
Kuna baadhi ya siku, safari fupi tu, kwa mfano kutoka Manzese hadi Posta, huwalazimu watumiaji wa barabara ya Morogoro kutumia hadi saa tatu ili kufika wanakokwenda. Adha ya foleni ni kubwa.
Ni dhahiri kuwa katika mazingira kama haya, usafiri wa pikipiki ndiyo suluhisho la pekee kwa wale wenye shughuli za dharura. Hivyo, Mamlaka za jiji kwa kushirikiana na vyombo vingine kama Mamlaka ya Udhibiti wa Usafiri wa Majini na Nchi Kavu (SUMATRA) na pia Jeshi la Polisi, vinapaswa kutambua kuwa huu si wakati mzuri wa kuzuia bodaboda kwenda katikati ya jiji na maeneo mengine pia.
Tunadhani vilevile kuwa, hata kama zuio hili likaendelea kubaki, basi ni vyema kukawa na utaratibu unaoeleweka wa kutofautisha waendesha bodaboda na watumiaji binafsi wa pikipiki.
Hali ya sasa si nzuri. Inawapa wananchi mateso na manyanyaso yasiyostahili kwa sababu wapo waliotozwa faini na kupotezewa muda wao mwingi barabarani kwa kudhaniwa kuwa ni watu wa bodaboda ilhali ukweli ni kwamba baadhi yao hubeba wake zao tu wakati wakiwahi kibaruani. Suala la usalama pia linahitaji ufafanuzi wa kina.
Hii ni kutokana na ukweli kuwa, kama bodaboda ni hatari kwa usalama katika maeneo ya Posta, basi hatari hiyo haiondoki pia katika maeneo mengine ya jiji kama Buguruni, Tegeta, Mwenge, Sinza, Kariakoo na Mbagala ambako pia kuna benki, maduka makubwa, ofisi za kampuni na shughuli nyingine za uzalishaji. Ni vyema amri hii ya kuzuia bodaboda katikati ya jiji ikatazmwa upya.
Tahadhari mvua kubwa,kimbunga visipuuzwe
KUNA tishio la kutokea mvua kubwa itakayoambatana na upepo mkali jijini Dar es Salaam na mikoa mingine ya Pwani ya Bahari ya Hindi ndani ya siku mbili zijazo.
Hii ni kwa mujibu wa taarifa ya utabiri wa hali ya hewa iliyotolewa na Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA).
NIPASHE tunashauri kuwa tahadhari hii isipuuzwe. Ifanyiwe kazi kuepuka maafa.
Kwa mfano, wakazi wa maeneo ya bondeni wanapaswa kuondoka mara moja.
Watumiaji wa vyombo vya majini wanapaswa kuwa makini pia katika siku hizi mbili ili kuepusha maafa ya kuzama kwa vyombo vyao kutokana na upepo mkali.
Shime, ile desturi ya kupuuza taarifa za wataalamu wa hali ya hewa iachwe mara moja. Ni hatari.
CHANZO: NIPASHE
Share:

0 maoni:

MATUKIO YA VIDEO

Recent Posts

Unordered List

Pages

Theme Support

Sample Text