Kumekuwa na malalamiko mengi kuhusiana na wizi wa fedha kwa njia za mtandao ambapo watu mbalimbali wamekuwa wakiibiwa kupitia simu zao, na hata akaunti za benki pia.
Leo Novemba 19 katika kikao cha Bunge Dodoma Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia January Makamba amesema haya; “..Wizi wa kupitia mitandao ya simu hauna tofauti na wizi na aina nyingine, kinachofanyika ni kuwa wahalifu wanatumia fursa za miamala ya kifedha kupitia mitandaoni kufanya uhalifu.. Wizara imekuwa ikipokea malalamiko kuhusu wizi wa fedha ama wa moja kwa moja kutoka kwenye akaunti za fedha za mtandao, au kutoka kwenye akaunti za benki kupitia huduma za simbanking..”
“..Kinachotokea ni kwamba wezi wanapata taarifa za mwenye akaunti ama kutoka kwa mwenye akaunti mwenyewe, au kwa njia nyingine na hivyo kuingia kwenye akaunti na kufanya miamala ikiwa ni pamoja na kuiba au kuhamisha fedha. Takwimu zinaonyesha kuwa katika kipindi cha mwezi wa kwanza mwaka 2012 hadi Septemba 2014 jumla ya matukio 999 ya makosa mbalimbali ya kimtandao yaliripotiwa katika vituo vya Polisi hapa nchini kwa mchanganuo ufuatao:-
- Mwaka 2012 kulikuwa na makosa 414
- 2013 kulikuwa na makosa 333
- Mwaka huu (2014) mpaka sasa kuna makosa 252.”
“..Jumla ya kesi 212 zenye watuhumiwa 132 zilifikishwa Mahakamani na kesi 787 ziko katika hatua mbalimbali za upelelezi.
Naomba nitumie fursa hii kuwaasa Watanzania wanaotumia huduma za aina yoyote ya kimtandao kujiepusha na kujibu maswali au kukubali masharti ambayo hawamjui anayeyatoa au anayatoa kwa nia gani, hii ni hatari mara nyingi kwa kutojua mwenye akaunti hutoa taarifa zake yeye bila kufahamu kuwa amefanya hivyo, ni muhimu kusoma kwa umakini na kufahamu nini unachokikubali vinginevyo ni muhimu kuomba msaada kutoka kwa watoa huduma.“– Makamba.
“..Kwa lengo la kuongeza usalama wa matumizi ya huduma za kimtandao Wizara imekamilisha miswada mitatu ya sheria za usalama mtandaoni, Cyber Security Laws. Ambazo ni; sheria ya kwanza, sheria ya kulinda taarifa binafsi, inaitwa Personal Data Protection, Ya pili ni sheria ya miamala ya kielektroniki, yaani Electronic Transaction Bill na ya tatu ni sheria ya kudhibiti uhalifu wa mtandao wa kompyuta, kwa maana Computer and Cyber Crime Act..”– Makamba.
Sheria hizi tumeshazipeleka kwenye Cabinet Secretariet na zitaletwa hapa Bungeni mwaka ujao…”- Makamba.
Kumsikiliza Naibu waziri huyo, bonyeza play hapa.
0 maoni:
Chapisha Maoni